Viongozi kutoka mrengo unaomuegemea naibu wa rais William Ruto wanamtaka rais Uhuru Kenyatta kuhakikisha miradi yote iliyosimamishwa katika ngome ya Naibu wake inafufuliwa.
Kundi hilo likiongozwa na gavana wa Turkana Josephat Nanok limesema kuwa limeridhishwa na miradi ya rais uhuru katika maeneo mbalimbali nchini na sasa wanaitaka miradi iliyosimama katika eneo la bonde la ufa pia iendelezwe.
Wakihutibia wanahabari baada ya mkutano wa majadiliano ya pamoja na viongozi kutoka eneo la bonde la ufa, viongozi hao wamesema kuwa miradi ya mabwawa mbalimbali iliyoanzishwa na serikali inapaswa kumalizwa kwa faida ya wananchi katika eneo hilo.
Mbali na miradi iliyokwama, viongozi hao wanaojumuisha magavana, maseneta, wabunge na wawakilishi wadi, vilevile waliweka wazi kuwa yapo mambo muhimu yanayohusu eneo hilo ambayo yatatakiwa kuongelewa na serikali itakayoundwa baada ya uchaguzi unaokuja.